Sunday, December 2, 2007

Maximo kwa hili hapa!!!!!!!



WIKIENDI ndio hiyo inajikata na mambo yake kibao ambayo ni mswano zaidi kwa wana wa Dasilamu ambao kwao hakuna linalokatiza bila kutestiwa sambamba na matanuzi kama kawa.
Ambao wameshaseti mambo yao wanatamani hata huyo Mkuu wa Kaya, angetangaza evuridei ni wikiendi tu ingawa wapo wanaolaani mambo yanavyokwenda kwa vile hali si hali.
Wanatamani hata kurudisha laifu ya enzi hizo kileji lakini ah wapi. Soli zinazidi kutoboka kutokana na mapambano na lami za kisasa walizotuwekea mpaka uswahili hao mnaowaita Tanrodi.
Washirika wako kwenye hesabu kali, kutafakari jinsi ya kufunga mambo na viwalo vya klithmasi. Unafanya mchezo nini ndio bongo hiyo?
Usione wenye suti zao wanamwagika jasho ukadhani ni msongamano wa kwenye daladala za Mwenge- Posta. Wenzio wamepiga mguu kutoka Posta Mpya mpaka Mwananyamala kwa Manjunju.
We hujasikia wenzio wanakuambia Mjini Shule ndio mambo hayo ya kiutu uzima, kinaeleweka kwa vyovyote vile hata kwa kusaga lami nani arudi kijiji kwenye vibatari wakati mishumaa ipo hata msikiti wa jirani au Chachi itaibwa Tanesco wakikwapua umeme wao.
Unafikiri wote wenye vitambi huko Dasilamu mjini ndio wala vyuku na bia huko Kempski? Wengine mambo ya Wali Maharage tu wa jero na maji ya fifte kwa Kariakoo tu.
Ndio tawni hiyo bro akili kichwani. Lakini nimeskia na jamaa yenu naye kaanza, akifanikiwa kuwarudisha tena Brazil safari hii atashindwaje kuwaambia kazaliwa Kishumundu?
Ameanza tena! hajui hata kama wengine tukikumbuka machungu ya kipigo cha 4-0 tulichokula Senegal miezi fulani iliyopita tukachanganyikiwa.
Lakini wiki hii baada tu ya kuiona ratiba ya kufuzu Sauzi kwenye kombe la Dunia 2010, yule yule Marcio Maximo kocha wetu huyo! Wa Stars ameanza hadithi za kambi ya Brazil.
Hivi kuna nini? Halafu anashikilia bango kana kwamba ndio kila kitu kipo huko na tusipokwenda tumekwisha. Ndio tunaheshimu kwamba angalau ameleta changamoto kwa wachezaji na mashabiki tangu aanze kufanya mambo Stars miezi kadhaa iliyopita, lakini kwa hili mimi hapana! No. Amekuwa akisisitiza wiki hii kwamba lazima airejeshe Stars mwakani, Brazili alikokuwa ameweka kambi kabla ya kuvaa na Senegal jijini Dakar.
Sababu zake ni kwamba anataka kwenda kumalizia programu aliyoianza Januari alipopiga kambi ya mwezi mmoja, tukapigwa fiksi kwamba tumetisha, wote hao Botafogo,Fluminence, Flamingo na Vasco da Gama wanatupigia saluti vibaya sana kutokana na kiwango.
Vasco da Gama, ambayo iliifunga Manchesta (hiyo ya Fagasoni) 3-0 eti Stars iliitesa mpaka ikaomba mpira uishe eti! jamani mtatudanganya mpaka lini?
Wanaofanya kazi kama ya Mzee wa Kutibua wakatuandikia 'makala za kufa mtu' kwamba Stars Kiboko, tishio Brazil, makocha wameivulia kofia na wengine wakathubutu kwenda mbaa...li eti na wachezaji wetu kina nanihii na wenyewe wamekuwa lulu wanasakwa kila kona.
Wamekuwa juu eti hata kuliko Wabrazil wenyewe ambao kila leo wanamwagika Ulaya, sembuse sisi ambao hata Uarabuni tunanyatia kuingia tena tukienda tunatisha kwenye mabonanza ya Machimbo?
Kimsingi sikubaliani hata kidogo na hoja za Maximo kuhusiana na uamuzi wake wa kupeleka timu Brazil kwa mara nyingine, wala sidhani kwamba kuna ulazima wa anachotaka kutushawishi tumuelewa, labda atumie nguvu nyingine sababu hata Tiefuefu yenyewe ambayo ndio inayopaswa kuratibu ishu kama hizo haijasikika ikichangia lolote kuhusiana na safari hiyo kitu ambacho kinanipa wasiwasi.
Yawezekana Maximo ana malengo, lakini si kwa uchumi wa Tanzania hii ya sasa. Januari alikuwa na kikosi cha Wanaume kama 25 ambao kwa makadirio ya haraka alitumia mil. 100 za wadhamini Brazil ambako baadaye tukafungwa na Senegal akapukutisha karibu nusu na kuita wapya.
Sasa hata kama ni programu ya muda mrefu ameandaa mbona wale aliokwenda nao mwanzoni amewapukutisha kiasi hicho na hata waliko hatuwasikii tena hata wanachofanya na kama atawaita tena kwa faida ya nani?
Muendelezo utatoka wapi wakati kikosi kilichopo kambini kina wachezaji kibao wapya, ina maana atakwenda kukaa miezi miwili tena aanze moja? mbona anatupa maswali magumu, au kuna kitu anatafuta Brazili?
Hata kama lengo lake ni kurejesha wale wa mwanzo akaendelee nao kwanini aliwaacha halafu sasa awaone lulu? Katika mkutano na waandishi alikiri amefanya mazungumzo na wadhamini kuhusiana na hilo. Hivi nini kazi ya Tiefuefu na maofisa wake kama mpaka Kocha ana nguvu ya kupita mpaka kupeleka muhtasari wake kwa mdhamini bila kuwahusisha?
Kwanini Maximo asiweke kambi ya muda mfupi kwenye nchi zenye kiwango cha juu Afrika na kucheza mechi kadhaa za kirafiki na timu imara kuliko kwenda kucheza mabonanza Brazil na klabu ambazo siamini zinaweza kutusaidia lolote hata tukikaa miezi sita!
Yatakuwa ni yale yale ya kucheza na timu C mwisho wa siku tunavimba vifua kwamba tunajua na kuunguza manoti kumbe wapi. Nchi za Afrika kwa mfano, Misri, Tunisia, Sudan,Ghana, Angola tukizitumia zinaweza kutujenga zaidi kuliko kukimbilia Brazil hata tukicheza na klabu kama Zamalek, Al-ahly, Al-Merrekh zinaweza kutusaidia kuliko kwenda kufanya mazoezi kwenye viwanja vya Brazil, naanza pengine kupata hata wasiwasi na washauri wa Maximo na uhusiano wake kimaamuzi na Tiefuefu ya Leodgar Tenga.
Isifike mahali wadhamini pia wakatuendesha wanavyotaka lazima Tiefuefu iwe na maamuzi na kuangalia hadhi ya timu ya Taifa na sababu za msingi za kila inapokanyaga timu hiyo, ni mali ya Watanzania hiyo si klabu ya wanachama 300 wanaoweza kukutana Msimbazi wakamng'oa Dalali au Jangwani wakamtosa Madega.
Lazima kuangalia faida, hasara mwisho wa siku nyie ndio mnaonekana hovyo, au tubaki kuamini kwamba Maximo anawaendesha kama tunavyosikia huku mtaani?

No comments: